Katika kijiji cha Matare
wilaya ya Mugumu Serengeti, bwana Wambura alikamatwa kwa kesi ya kusingiziwa na
kuhukumiwa kwenda jela miaka mitatu, huku nyuma akiacha mke na watoto wanne
waliokuwa wanasoma. Hukumu hiyo ilimtesa sana kichwa chake, alitamani kila mtu
anayemhisi kuwa ana makosa aingie katika moyo wake na kuupata ukweli.
Alilia na
umaskini wake, labda angepata wakili mzuri angeweza kumtetea, kumkosa wakili
kukahalalisha kifungo hicho!! Alikwenda gerezani huku akiumia sana rohoni.
Aliyaanza maisha mapya kwa
shida sana, akawa mnyonge kila mara na mwili ukapoteza afya kiujumla. Huko
gerezani alifanikiwa kupata rafiki aliyekuwa na cheo ama jukumu la uzikaji wa
wafungwa hasahasa ambao hawakuwa na ndugu ama ambao ndugu zao huwa hawajitokezi
pale gerezani.
Mzikaji alijaribu sana kumtia nguvu Wambura na kumwaminisha kuwa
hiyo ilikuwa hatua tu ya maisha anapaswa kuizoea na siku moja ukweli
utajulikana tu! Bwana Wambura maneno ya mzikaji hayakumuingia kabisa...alizidi
kunyong’onyea. “Siwezi kuvumilia kukaa gerezani miaka mitatu…..kama unajali
kilio changu nisaidie nitoroke kwa namna yoyote ile ndugu yangu!!” Wambura
alimsihi mzikaji.
SIKU MOJA mzikaji akamwambia
Wambura kuwa msaada umepatikana. Lakini yataka moyo!! “Nipo tayari kwa lolote
ilimradi tu nitoke humu!!” alijibu kwa msisitizo huku akimtegea sikio mzikaji.
“Msaada pekee wa kukutorosha humu ndani ni kwa njia ya jeneza… yaani mfungwa
akifa mimi nakuunganisha naye kwenye jenerza…..” akashusha pumzi kisha akaendelea
“Wewe ukisikia kengere ya msiba, njoo mara moja kwenye chumba cha maiti,
utakuta tayari sanduku liko katikati ya chumba linakuwa halijafungwa, funua
kifunioko ingia ndani yake ulale pembeni ya maiti kwani sanduku huwa kubwa la
kutosha kila aina ya maiti na hata miili miwili inaingia. Kisha nitakuja na
kulipigilia misumari. Baada ya muda tutalipakia kwenye gari na kutoka kwenda
nje ya gereza makaburini nikiongozana na baadhi ya wafungwa na maaskari
magereza. Tutakuzika huko lakini baada ya dakika 20 hadi 30 nitarudi kukufukua.
Hautaweza kushindwa kupumua kwa dakika hizo, utatoka ukiwa huru.”
JAPOKUWA wazo
lilikuwa zuri lakini lilimtisha sana Wambura. Hata hivyo akaona afadhali afanye
hivyo kuliko kukaa gerezani miaka mitatu bila kosa.
Siku moja akasikia kengere ya msiba. Akafanya
kama alivyoelekezwa na mzikaji. Akaenda na kuingia chumba cha maiti. Kweli
akalikuta sanduku, akiwa na hofu kuu akaingia na kulala pembeni ya maiti
iliyokuwepo. Mara akasikia mtu ameingia na kulipigilia msumari sanduku. Muda
mfupi baadaye sanduku likainuliwa na kuwekwa kwenye gari. Gari ikatoka nje ya
gereza hadi makaburini. Sanduku likashushwa na kuwekwa kaburini na kuanza
kufukiwa. Wambura alijitahidi sana kuvumilia japo hofu ilizidi kutanda.
Alimtegemea sana mzikaji na alianza kumuona mkombozi wa maisha yake. Kama
alivyoambiwa, akasubiri dakika kumi, ishirini.. zikapita kimya!! Dakika
thelathini kimya. Joto nalo likazidi kuongezeka. “Nitavumilia hadi afike…”
alijisemea kisha akajiongezea kauli ya ujasiri. “Kama nilitakiwa kuishi
gerezani miaka mitatu kivipi dakika kadhaa za hapa kaburini”
KWA kuwa alishakaa
gerezani kwa muda kiasi akatamani kujua aliyekufa ni nani… ni kwewli aliogopa
kuitazama maiti lakini aliona kama inatisha zaidi ikiwa imefunikwa vile kuliko
ikiwa wazi. Akaifunua upande wa usoni… Kwa kuwa kulikuwa na giza nene alikodoa
sana macho kuitazama. LAHAULA!!! MACHO YAKAKUTANA NA SURA YA MZIKAJI!!! MZIKAJI
ALIKUWA AMEKUFA NA AMEZIKWA NA AHADI ZAKE ZA UKOMBOZI!!
FUNZO:: Usimtegemee sana
mwanadamu katika maisha yako, kwanza ni dhambi!! Pili mwanadamu anakumbana na
vikwazo kama unavyokumbana navyo wewe hadi kumwendea yeye. Hivyo kumpatia
maisha yako ni kuzidi kuyaweka hatarini zaidi!! Umeonewa umesingiziwa
unanyanyaswa….. mwachie Mungu afanye maamuzi…
Haya mzikaji
aliyetegemea atamfukua naye ni maiti…… tazama mateso atakayoyapata hadi kufa
kwake….. Bila shaka atatamani kurudi gerezani kwa miaka mingine kumi lakini
haitawezekana tena!!!